Skip to content

Serikali yatoa ruhusa viwanja vipya kutumika

NA MWAJUMA MMANGA

WIZARA ya Habari,Sanaa,Utamaduni na Michezo Zanzibar,imesema inaendelea kutoa ruhusa ya viwanja vya michezo kwa utaratibu mzuri lengo kuvitunza viwanja hivyo.

 Naibu wa waziri wa wizara hiyo Ali Abdulgullam Hussein,aliyasema hayo huko Chukwani alipokuw akijibu suala la nyongeza lililoulizwa na mwakilishi wa jimbo la Mtambwe Dk. Mohammed Ali Suleiman,aliyetaka kujua juu ya kuwawezesha vijana   waliokuwa hawana uwezo wa kulipa viwanja wakati wanapotaka kutumia.

Alisema  serikali inatoa ruhusa kwa kila mtu kutumia viwanja,ikiwemo vya Maisara na Mao ambapo hivi karibu katika viwanja vya Mao kulikuwa na ligi ya Mapinduzi Cup kwa  upande wa timu za akademi.

Alisema serikali inaendelea kutoa ruhusa kwa viwanja vya Mao ambapo hufanyika  mashindano ya mechi za vijana. 

 Alisema lengo la serikali kutoa ruhusa hiyo ni kuona vijana wanapata nafasi ya kutumia viwanja hivyo na kuonyesha vipaji ili kuwa wachezaji bora wa baadae.

Alisema wana malengo ya kutafuta msimamizi wa  viwanja hivyo ili kuhakikisha kila mmoja anapata nafasi ya kutumia.

Gullam alisema viwanja vya Maisara vilifungwa kwa sababu ujenzi haujakamilika,lakini hivi sasa vimekamilika  na vinatumika.

Akijibu suala la msingi,lililouliza na mwakiishi huyo huyo,aliyetaka kujuwa sababu zinazofanya viwanja vya Maisara kufungwa,jambo ambalo linawakosesha vijana kukushindwa kutumika.

 Alisema sababu za kutotumika kwa baadhi ya viwanja ni kunatokana na hatua  mbalimbali za uwekezaji ,ikiwemo kutokamilika kwa ujenzi,kutokabidhiwa rasmi na kutopangiwa utaratibu wa matumizi na uendeshaji.

Alisema serikali inaendelea  kushughulikia hatua hizo na mara baada ya  viwanja vinapokamilika  hukabidhibiwa na kupangwa utaratibu  wa uendeshaji,kufunguliwa pamoja na kutumika kwa madhumuni ya kuwahudumia vijana  kama ilivyokusudiwa.

Alikitoa ufafanuzi juu ya viwanja vya Maisara ,alisema viwanja hivyo vitaendelea kutumiwa na wananchi wote wakiwemo  waliokuwa wakivitumia  kabla ya kufanyiwa marekebisho.