Skip to content

Boti iliyobeba  wahamiaji yapinduka wengi wahofiwa kufariki

ROMA, ITALIA

BOTI iliyokuwa na wahamiaji 51 ilipinduka katika bahari ya Mediterania hivi majuzi, huku mmoja akithibitishwa kuwa hai na 50 bado hawajapatikana, vyombo vya habari vya ndani viliripoti.

Mtu pekee aliyenusurika aliokolewa na meli ya wafanyabiashara na kusafirishwa hadi hospitali ya Malta kwa matibabu.

Kulingana na manusura, boti hiyo ilisafiri kutoka Libya siku ya Alhamisi na kupinduka siku iliyofuata. Mtu aliyenusurika alishikilia sana mabaki ya chombo walichosafiria na kuelea juu ya maji kabla ya kuokolewa.

Baada ya ajali hiyo, shughuli za utafutaji na uokoaji zilianzishwa, na watu 50 walikuwa bado hawajapatikana.

Takwimu za Shirika la Kimataifa la Uhamiaji (IOM) zilionyesha kuwa watu 14 wametoweka au kuthibitishwa kufariki katika bahari ya Mediterania tangu mwanzoni mwa mwaka huu. Idadi ya vifo na kupotea ilifikia 1,873 kwenye njia hiyo mnamo 2024.